ADEM Logo
JAMHURI YA MUUNGANO WA TANZANIA

TUME YA HAKI ZA BINADAMU NA UTAWALA BORA

Tunajenga utamaduni wa kuheshimu haki za binadamu, misingi ya utawala bora na utu wa mtu
ADEM Logo

VIONGOZI THBUB   WASHIRIKI MAFUNZO YA HAKI ZA BINADAMU NCHINI INDIA

26 Mar, 2025
VIONGOZI THBUB   WASHIRIKI MAFUNZO YA HAKI ZA BINADAMU NCHINI INDIA

 

Kamishna wa Tume za Haki za Binadamu, Mhe. Nyanda Shuli akiambatana na Katibu Msaidizi wa Tume Bw. Juma  Karibona na Mkurugenzi wa Elimu kwa Umma, Mawasiliano , Tafiti na Nyaraka, Bi. Monica Mnanka ni miongoni mwa Viongozi kutoka  Taasisi za Kitaifa za Haki za Binadamu kutoka nchi 11 ambao wamepata mafunzo kuhusu haki za binadamu nchini India hivi karibuni. 

Mafunzo hayo yaliyolenga kuzijengea uwezo taasisi hizo katika kulinda na kuhifadhi haki za binadamu yalifanyika katika Chuo cha Utumishi wa Umma kwa ufadhili wa Tume ya Haki za  Binadamu ya India ikishirikiana na Wizara ya Mambo ya nje ya  nchi hiyo kuanzia Machi 03 hadi 08, 2025

Katika kipindi hicho, viongozi hao walijifunza kuhusu  masuala ya haki za binadamu yanayoendelea kujitokeza katika zama hizi zilizotawaliwa na maendeleo makubwa ya teknolojia, ulinzi wa haki za  makundi maalum katika jamii,  nafasi ya mtandao na haki za binadamu, upatikanaji wa huduma za afya,  demokrasia   na chaguzi huru vinavyohusiana na haki za binadamu.

Mambo mengine waliojifunza ni pamoja na  jinsi ya kushughulikia malalamiko, uvunjifu wa haki za binadamu,  uchunguzi, ushirikiano wa Tume  na Asasi za kiraia katika kutetea haki za binadamu na uchambuzi wa taarifa za haki za binadamu.

Katika mafunzo hayo, nchi wenyeji India waliweza kueleza namna ambavyo imeweza kuhifadhi haki za binadamu nchini humo, kujengea uwezo nchi  nyingine katika kuhifadhi haki hizo na namna inavyoshirikiana na asasi na  jumuia mbalimbali katika kuhakikisha haki za binadamu zinalindwa na kuhifadhiwa.

Utoaji wa mafunzo ya kuwajengea uwezo viongozi wa Taasisi za Kitaifa za Haki za Binadamu kutoka  nchi mbalimbali ni moja ya mafanikio ambayo nchi ya India inajivunia kwa kutumia uzoefu wake katika ulinzi na utetezi wa haki za binadamu ndani na nje ya mipaka ya nchi yao pamoja na kuwezesha washiriki kubadilishana uzoefu.